Lionel Messi ameendelea kuandika historia baada ya kufunga mabao mawili na kuiongoza Inter Miami kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Atletico San Luis katika mchezo wa ufunguzi wa hatua ya makundi wa michuano ya Leagues Cup 2026 uliochezwa nyumbani kwao.
Kwa mabao hayo mawili, Messi amefikisha jumla ya mabao 14 katika historia ya Leagues Cup, rekodi inayomfanya kuwa mfungaji bora wa muda wote wa mashindano hayo yanayozikutanisha klabu za Major League Soccer (MLS) na Liga MX ya Mexico.
Atletico San Luis ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao kupitia David Rodriguez dakika ya nne, kabla ya Messi kusawazisha dakika saba baadaye. Kiungo wa Venezuela, Telasco Segovia, aliifungia Inter Miami bao la pili dakika ya 26 na kuwapa wenyeji uongozi.
Messi aliongeza bao lake la pili muda mfupi kabla ya mapumziko, huku beki wa Brazil, Micael, akifunga bao la nne katika dakika za nyongeza za kipindi cha kwanza. Rafa Llorente aliifungia Atletico San Luis bao la kufutia machozi kipindi cha pili na kufanya mchezo kumalizika kwa ushindi wa mabao 4-2 kwa Inter Miami.
Katika michezo mingine ya Leagues Cup iliyochezwa Jumatano, FC Dallas iliichapa Queretaro mabao 2-0, huku Club Leon ikiibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Nashville SC.


