Nyota wa Brazil, Neymar Jr, atakosa mechi mbili zijazo za kirafiki za timu ya taifa hiyo baada ya kuthibitishwa kuwa na majeraha ya daraja la pili kwenye misuli ya mguu wa kulia.
Daktari wa timu ya taifa ya Brazil, Rodrigo Lasmar, alithibitisha taarifa hiyo Alhamisi na kueleza kuwa mshambuliaji huyo atahitaji wiki mbili hadi tatu kupona kabisa.
Bila kusahau meridianbet ndio wakali wa ODDS KUBWA, Machaguo zaidi ya 1000 na kila kitu ukitakacho. Bashiri kijanja hapa
Kutokana na majeraha hayo, Neymar hataichezea Brazil katika michezo ya kirafiki dhidi ya Panama itakayopigwa Jumapili, Mei 31 pamoja na mchezo dhidi ya Misri utakaochezwa Juni 6. Majeraha hayo pia yanaweka mashakani uwepo wake kwenye mchezo wa kwanza wa Brazil katika Kombe la Dunia dhidi ya Morocco.
“Sio uvimbe wa kawaida pekee,” alisema daktari Rodrigo Lasmar wakati akizungumzia hali ya Neymar, akiongeza kuwa maendeleo ya nyota huyo yataendelea kufuatiliwa kwa karibu katika wiki zijazo kabla ya uamuzi wa mwisho kuhusu ushiriki wake kwenye mchezo wa ufunguzi wa Kombe la Dunia.
Taarifa za majeraha hayo zimekuja siku moja baada ya Neymar kukosa mazoezi rasmi ya kwanza ya Brazil yaliyofanyika katika kambi ya Granja Comary, Teresopolis. Mshambuliaji huyo alipelekwa katika kliniki ya karibu kwa ajili ya vipimo zaidi baada ya kuonekana akiwa na uvimbe kwenye eneo la ndama wa mguu wake.
Inaelezwa kuwa tatizo hilo lilianza Mei 17 wakati Neymar alipohisi maumivu katika mchezo ambao klabu yake ya Santos ilifungwa mabao 3-0 dhidi ya Coritiba kwenye Ligi Kuu ya Brazil. Tangu siku hiyo, hajarejea mazoezini akiwa na mpira jambo lililoibua hofu kubwa ndani ya kambi ya Brazil kuelekea Kombe la Dunia.
Kukosekana kwa Neymar ni pigo kubwa kwa Brazil ambayo ilikuwa ikimtegemea nyota huyo katika maandalizi ya mwisho kuelekea michuano ya Kombe la Dunia. Mashabiki wa soka nchini humo sasa wanasubiri kuona kama mshambuliaji huyo mwenye jezi namba 10 ataweza kurejea kwa wakati kabla ya mchezo wa kwanza wa Brazil dhidi ya Morocco.


