Mwamuzi maarufu wa England, Anthony Taylor, ametangaza rasmi kustaafu kuchezesha soka la kiwango cha juu, akihitimisha safari ya zaidi ya miaka 20 iliyomshuhudia kuchezesha jumla ya mechi 831 katika mashindano mbalimbali ya ndani na kimataifa.
Taylor mwenye umri wa miaka 47 amechezesha mchezo wake wa mwisho katika michuano ya Dunia, ambapo alisimamia mechi ya hatua ya 16 bora kati ya Ureno na Hispania nchini Marekani. Uamuzi huo unahitimisha moja ya kazi zilizotukuka zaidi kwa mwamuzi katika historia ya soka la England.
Katika kipindi chake cha uamuzi, Taylor alichezesha fainali zote kubwa za mashindano ya ndani nchini England, zikiwemo Fainali za Kombe la FA mwaka 2017 na 2020, Kombe la Ligi mwaka 2015, Community Shield mwaka 2015 pamoja na fainali ya mchujo wa Championship mwaka 2018.
“Kuchezesha soka la kiwango cha juu imekuwa heshima kubwa kwangu, lakini shinikizo ni kubwa na uchunguzi wa kila uamuzi haukosekani. Nafikiri huu ndio wakati sahihi wa kuondoka na kuanza ukurasa mpya wa maisha yangu,” alisema Taylor katika taarifa yake.
Mbali na mafanikio yake nchini England, Taylor alidumu kwa miaka 14 kwenye orodha ya waamuzi wa kimataifa ya FIFA na alichezesha mashindano makubwa duniani, yakiwemo mashindano ya Dunia la 2022 na 2026, Euro 2020 na 2024, pamoja na michuano ya Dunia la Klabu la FIFA mwaka 2022 na 2025, akijijengea sifa kama mmoja wa waamuzi bora zaidi kuwahi kutokea England.


