Michuano ya AFCON barani Afrika inazidi kupamba moto huko Morocco ambapo timu kadhaa zimeanza vyema na zingine zikianza vibaya ikiwemo Tanzania ambapo walipigika kwa mabao 2-1 dhidi ya Nigeria mechi iliyopigwa katika dimba la Fez mjini Fez nchini Morocco.

Mabao ya Super Eagles yamefungwa na beki wa Hull City ya England, Oluwasemilogo Adesewo Ibidapo “Semi” Ajayi dakika ya 36 na winga wa Atalanta ya Italia, Ademola Lookman Olajade Alade Ayoola Lookman dakika ya 52, wakati la Taifa Stars limefungwa na kiungo wa Floriana ya Malta, Kokola Charles William M’Mombwa dakika ya 50.
Kipigo hicho ni mwendelezo wa ubabe wa Nigeria kwa Tanzania kwenye Fainali za AFCON na mashindano yote kwa ujumla.
Mara ya kwanza timu hizo kukutana kwenye Fainali za AFCON ilikuwa ni mwaka 1980 na Nigeria wakiwa wenyeji waliibuka na ushindi wa mabao 3-1 Machi 8 Uwanja wa Surulere Jijini Lagos.
Zaidi ya hapo timu hizo zimekutana mara mbili katika mechi za Kundi G kufuzu AFCON ya 2017, Super Eagles ikiendeleza ubabe kwa ushindi wa 1-0 nyumbani Septemba 3 mwaka 2016 bao la Kelechi Iheanacho dakika ya 79 wakati huo akitokea Manchester City na huo ulikuwa mchezo wa marudiano baada ya taifa Stars kulazimishwa suluhu (0-0) Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam Septemba 5, mwaka 2015.



