Kikosi cha wachezaji 22, viongozi pamoja na benchi la ufundi wataondoka Jijini Dar kesho kuelekea Mbarali mkoani Mbeya kwenye mchezo wa Ligi kuu ya NBC dhidi ya Ihefu utakaopigwa Januari 3, mwaka huu.
Akizungumzia maandalizi yao, Ofisa Habari wa KMC, Christina Mwagala amesema kuwa kikosi kipo tayari kwa ajili ya mapambano ya kuhakikisha wanarejea na pointi tatu muhimu.
“Tumetoka kupoteza mchezo wetu dhidi ya Simba siku ya Desemba 26, mwaka huu lakini bado tupo kwenye ari na morali nzuri kwa sababu ni sehemu ya matokeo kwenye mpira wa miguu, hatupaswi kurudi nyuma badala yake tumejikita zaidi kusonga mbele kwenye michezo iliyopo mbele yetu hivi sasa.
“Tunapokwenda Mbarali tunafahamu kuwa tutakuwa na mchezo mgumu na wenye ushindani kwani Ihefu wamekuwa na wakati mzuri kwenye matokeo, na kwamba sisi KMC tumejiandaa vya kutosha ili kuhakikisha kwamba alama tatu muhimu zinapatikana.
“Kwa upande wa Afya za wachezaji, wote wapo kwenye hali nzuri, bado KMC itaendelea kukosa huduma za wachezaji wake muhimu wawili ambao ni Hance Masoud pamoja na Emmanuel Mvuyekure ambao bado wanaendelea kupatiwa matibabu kutokana na majeraha waliyoyapata mwezi mmoja uliopita.”
KMC FC inaenda kwenye mchezo wa mzunguko wa 19 kabla ya kuanza kwa mapumziko ya kupisha michuano ya kombe la mapinduzi ikiwa kwenye nafasi ya tisa, huku ikicheza jumla ya michezo 18 na kukusanya pointi 22 katika msimamo wa Ligi Kuu.