INGIZO jipya ndani ya kikosi cha Simba, Habib Kyombo ameweka rekodi yake Uwanja wa Mkapa kwa kuwa mzawa pekee aliyetupia wakati ubao wa Uwanja wa Mkapa ukisoma Simba 8-0 Eagle FC.
Ulikuwa ni mchezo wa Kombe la Shirikisho la Azam Sports raundi ya pili ambapo chini ya Kocha Mkuu, Juma Mgunda, Simba ilifanikiwa kutinga hatua ya 32 bora.
Katika mabao hayo nane yaliyofungwa juzi na timu hiyo, wachezaji wakimataifa walifunga mabao saba ambapo mawili yalifungwa na kiungo Clatous Chama dakika ya 30 na 73 na alitoa pasi mbili za mabao dakika ya 9 na 18.
Moses Phiri ambaye ni raia wa Zambia kama ilivyo kwa Chama, alifunga mabao manne akifunga hat trick ya mapema zaidi kwenye Kombe la Shirikisho ilikuwa dakika ya 14 kwa penalti, dakika ya 18, dakika ya 23 na dakika ya 60 huku akitoa pasi ya bao dakika ya 30.
Bao la saba kwa wachezaji wa kigeni lilifungwa na Pape Sakho aliyefunga bao hilo dakika ya 28 kutokana na mpira aliokutana nao ndani ya 18 uliotoka kuokolewa na mabeki wa Eagle na alitoa pasi moja ya bao dakika ya 23.
Kyombo ni mzawa pekee aliyefunga bao huku wazawa wengine wawili wakihusika kwenye kutoa pasi za mabao ambao ni Mohamed Hussein ‘Zimbwe Jr’ dakika ya 60 na Kibu Dennis dakika ya 73.