MKUDE, BOCCO WAONDOLEWA SIMBA

Kiungo mkongwe ndani ya Simba, Jonas Mkude leo anatarajia kuukosa mchezo wa ligi dhidi ya Namungo unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa kutokana na kutokuwa fiti.

Mbali na Mkude, pia nahodha John Bocco, Peter Banda, Nelson Okwa,Jimsony Mwanuke,Israel Mwenda hawa hawajawa fiti na Clatous Chama anatamatisha adhabu yake ya kufungiwa mechi tatu wanatarajiwa kukosekana kwenye mchezo wa leo na kufanya mastaa 7 kuwa jukwaani.

Juma Mgunda, Kocha Mkuu wa Simba amesema kuwa bandika bandua ya mechi za ushindani pamoja na ugumu wa ligi unampa kazi kwenye kupanga kikosi kutokana na kuwa na wachezaji wengi ambao hawapo fiti.

“Okwa bado majeruhi, Jimsony bado majeruhi, Mwenda ameanza mazoezi juzi Mkude naye ni mgonjwa, Bocco ni mgonjwa ameanza mazoezi hivi karibuni.

“Mnapocheza karibukaribu silaha kubwa ni kuwa na kikosi kipana chenye watu wazima wenye afya na akili, unapokuwa na kikosi kipana ambacho kina majeruhi hii bandika bandua utaona utamu wake na mimi nipo kwa wanaonja utamu huo.

“Ukishakuwa na kikosi bora na imara unafanya mabadiliko unavyotaka na kwa ligi hii ni lazima uwe na kikosi kipana wachezaji watakuwa wanaleta nafasi ya kushindana,”alisema Mgunda.

Kwa upande wa Kocha Msaidizi wa Namungo, Shadrack Nsajigwa alisema kuwa wamekuja kuchukua pointi tatu dhidi ya Simba na hawana majeruhi.

“Tunawaheshimu wapinzani wetu tunajua kwamba utakuwa mchezo mgumu lakini sisi hatuna majeraha,”

Acha ujumbe