Klabu ya Simba ambayo inaongozwa na kocha mkuu Robertinho imepokea kichapo cha mabao 3-1 dhidi ya Raja Casablanca kwenye mchezo wao wa marudiano hapo jana.
Mchezo huo ulipigwa majira ya saa 7:00 usiku kwa saa za Afrika Mashariki huku Simba wakimkosa beki wao Mohamed Hussein ambaye alikuwa na kadi tatu mfululizo za njano kwenye michuano hiyo.
Mechi ya kwanza vijana wa Msimbazi walichezea kichapo cha mabao 3-0, na jana licha ya kufungwa matatu walifanikiwa kupata bao 1 la kufutia machozi ambalo lilitupiwa kimyani na Jean Baleke.
Baada ya kupoteza mchezo huo mnyama amesalia nafasi ile ile ya pili akiwa na pointi zake 9, wakati kwa upande wa Raja Casablanca yeye bado ndiye kinara wa kundi hilo akiwa na pointi zake 16.