Bingwa wa kihistoria wa Kombe la CECAFA Kagame, Simba imejikuta ikianza kupiga hesabu za vidole kufuzu hatua ya nusu fainali baada ya kutoka suluhu ya pili mfululizo, safari hii ikiwa dhidi ya Jamus SC ya Sudan Kusini kwenye Uwanja wa Kigali Pele, Kigali.
Kufuatia matokeo hayo, Wekundu wa Msimbazi wamefikisha pointi mbili pekee na kuacha hatma yao mikononi mwa mechi ya mwisho ya hatua ya makundi.
Kocha Steve Barker alianza mchezo huo akiwa amefanya mabadiliko kadhaa kwenye kikosi chake huku Mothusi Cooper, ambaye yupo kwenye majaribio, akiwa miongoni mwa walioanza.
Wachezaji wengi waliokuwa tegemeo la kikosi cha kwanza walianzia benchi. Kipindi cha pili Barker aliongeza nguvu kwa kufanya mabadiliko manne kwa wakati mmoja, akiwaingiza Keletso Makgalwa, Ibrahim Doumbia, Yusuph Kagoma na Rushine De Reuck, kabla ya baadaye kuwaingiza Nickson Kibabage na Libasse Guaye.
Mabadiliko hayo yaliifanya Simba kutawala sehemu kubwa ya kipindi cha pili, lakini ilishindwa kutumia nafasi ilizozitengeneza na kupata bao la ushindi.



