Beki wa Barcelona, Eric Garcia, alitolewa kwa kadi nyekundu baada ya kumuangusha Alexander Sorloth alipokuwa akikimbilia kufunga bao katika dakika za mwisho, jambo lililopunguza nafasi ya timu hiyo kupata bao la tatu na kulazimisha muda wa ziada.
Atletico, ambao hawajawahi kushinda mashindano hayo na walipoteza fainali za mwaka 2014 na 2016 chini ya Diego Simeone, watakutana na Arsenal au Sporting Lisbon katika nusu fainali.
“Tuna furaha sana, tumewaondoa Barcelona ambao ni timu kubwa. Tulicheza vizuri ugenini… mwanzo ulikuwa mgumu sana kwetu, lakini timu ilijua jinsi ya kurejea mchezoni,” alisema kiungo wa Atletico, Koke, akizungumza na Movistar.
Barcelona walishinda mara ya mwisho Ligi ya Mabingwa mwaka 2015 na bado wanasubiri taji lao la sita, lakini kiungo Frenkie de Jong alisema klabu iko kwenye mwelekeo sahihi licha ya kuondolewa.
“Nadhani tulicheza vizuri sana, tulijitoa kwa kila kitu uwanjani, tulijaribu kila njia.Nahisi bahati haikuwa upande wetu. Tunapaswa kuendelea tuko kwenye njia nzuri, tunakua kila mwaka.” alisema mholanzi huyo.
Kocha wa Barcelona, Hansi Flick, aliwaweka benchi washambuliaji Marcus Rashford na Robert Lewandowski na kuwapa nafasi Ferran Torres na Gavi, akilenga kuisukuma Atletico kwa presha kubwa katika mchezo wa sita kati ya timu hizi msimu huu.

Mlinda mlango Juan Musso aliokoa kwa ustadi shuti la Lamine Yamal kwa kulipeleka pembeni ya lango sekunde 32 tu tangu kuanza, huku Barcelona wakianza kwa kasi katika mazingira ya uwanja wa Metropolitano uliokuwa na presha kubwa.
Kijana huyo Yamal aliwapa wageni uongozi mapema dakika ya nne baada ya kumlazimisha Clement Lenglet kupoteza mpira. Ferran Torres alimrudishia mpira Yamal ambaye alipiga shuti la chini lililopita katikati ya miguu ya Musso.
Dani Olmo alikaribia kuongeza bao la pili lakini Musso aliokoa tena, huku Barcelona wakiendelea kutawala mchezo.
Antoine Griezmann alipiga shuti lililotoka nje kidogo, Atletico wakionyesha dalili za hatari kupitia Ademola Lookman ambaye alimpa wakati mgumu Jules Kounde.
Barcelona waliongeza bao la pili dakika ya 24 kusawazisha matokeo ya jumla, Torres akimtoroka Lenglet na kufunga baada ya kupokea pasi ya Olmo.
Fermin Lopez angeweza kufunga la tatu lakini Musso aliokoa kichwa chake, huku kiungo huyo akipata jeraha usoni baada ya kugongwa na kiatu cha mlinda mlango huyo.
Atletico walirejea mchezoni dakika ya 31 baada ya Barcelona kupoteza umakini. Marcos Llorente alikimbia upande wa kulia na kutoa pasi kwa Lookman aliyefunga.

Barcelona walikatishwa tamaa mwanzoni mwa kipindi cha pili baada ya bao la Torres kukataliwa kwa kuotea.
Flick aliwaingiza Rashford na Lewandowski kutafuta bao lililohitajika, huku kipa Joan Garcia akiokoa kwa mguu wake dhidi ya Robin Le Normand.
Matteo Ruggieri alitoka damu baada ya kugongwa kiwiko na Gavi, hali iliyoonyesha presha kubwa uwanjani.
Mchezo uligeuka dhidi ya Barcelona pale Eric Garcia alipotolewa nje kwa kumchezea vibaya Sorloth alipokuwa anakwenda kufunga, tukio lililofanana na kadi nyekundu ya Pau Cubarsi katika mechi ya kwanza.
Flick alimpeleka mbele beki Ronald Araujo katika dakika za mwisho, lakini haikusaidia. Atletico walijikaza hadi dakika nane za nyongeza zilipoisha kabla ya kuanza kusherehekea ushindi wao.