Baada ya tetesi za kuhusishwa na Galatasaray, sasa imeripotiwa kuwa kiungo wa Napoli, Kevin De Bruyne, ambaye hajaridhishwa na hali ilivyo klabuni, anawindwa na klabu za Inter Miami, Chicago Fire na San Diego FC zinazoshiriki Ligi Kuu ya Marekani (MLS).

Nahodha huyo wa kimataifa wa Ubelgiji ameripotiwa kuvunjika moyo akiwa Napoli, baada ya kupambana na majeraha msimu uliopita na pia kumkosoa hadharani aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Antonio Conte. Aidha, inaelezwa kuwa uhusiano wake na kocha mpya Massimiliano Allegri nao hauonekani kuwa mzuri zaidi.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 35 alichagua kujiunga na Napoli kama mchezaji huru msimu uliopita, kwa kiasi kikubwa kutokana na uamuzi wa maisha binafsi baada ya kutumia muongo mmoja akiwa na Manchester City.
Kwa mantiki hiyo, inaaminika kwamba hatua yake inayofuata katika maisha yake ya soka pia itazingatia zaidi mtindo wa maisha kuliko sababu nyingine.
Galatasaray ilikuwa imetajwa kama moja ya klabu zinazoweza kuwasilisha ofa kwa Kevin De Bruyne, lakini kwa mujibu wa Mundo Deportivo, uwezekano mkubwa zaidi ni kwamba ataelekea kucheza katika Ligi Kuu ya Marekani (MLS).
Vilabu vya San Diego FC na Chicago Fire vinaonyesha nia ya kumsajili kiungo huyo wa Ubelgiji, lakini vinatajwa kuwa nyuma ya Inter Miami, ambao ndio wanaopewa nafasi kubwa zaidi ya kumpata.



