Napoli wanaendelea kufanya kazi ya kumfunga mkataba mpya Scott McTominay, huku rais wa klabu hiyo Aurelio De Laurentiis akiwa na nia ya kuondoa kabisa mashaka yoyote kuhusu mustakabali wa kiungo huyo katika Uwanja wa Stadio Diego Armando Maradona.

Kiungo huyo wa kimataifa wa Scotland amekuwa sehemu muhimu sana ya kikosi hicho tangu alipojiunga kutoka Manchester United mwaka 2024, ambapo amekuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya klabu hiyo ikiwemo kutwaa ubingwa wa Scudetto, na kujijengea nafasi ya kuwa miongoni mwa wachezaji wa kwanza kuanza kikosi.
Hali hiyo inatarajiwa kuendelea hata msimu ujao, licha ya kuondoka kwa kocha Antonio Conte na kuwasili kwa Massimiliano Allegri kuchukua mikoba ya ukocha.
Kwa mujibu wa Calciomercato.it, kiungo huyo mwenye umri wa miaka 29 anatarajiwa kukutana na mkurugenzi wa michezo Giovanni Manna pamoja na rais Aurelio De Laurentiis katika wiki zijazo ili kujadili kuongeza mkataba wake, ambao kwa sasa unaendelea hadi Juni 2028.



