Kwa mujibu wa La Gazzetta dello Sport, Liverpool wanakataa kushusha bei yao ya euro milioni 30 kwa ajili ya Curtis Jones, lakini Inter bado wana imani ya kufikia makubaliano na Reds, kwani kiungo huyo wa Uingereza ana nia ya kuhamia San Siro.
Inter wanaendelea kusukuma kwa nguvu usajili wa kiungo huyo wa Liverpool na wanaamini kwamba watafikia makubaliano na klabu hiyo ya Uingereza katika siku zijazo za karibu.
Gazeti la Gazzetta linaripoti kuwa Inter waliwasilisha ofa ya awali ya euro milioni 20 kwa ajili ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 mapema wiki hii, lakini Liverpool wanaendelea kung’ang’ania kiasi cha euro milioni 30 pamoja na kipengele cha kupata asilimia ya mauzo ya baadaye (sell-on clause).
Nerazzurri wanaripotiwa kufanya kazi ya kukamilisha dili hilo katika siku zijazo za karibu, huku wakitarajia Jones aweze kuanza maandalizi ya msimu mpya chini ya kocha Cristian Chivu ndani ya muda wa chini ya mwezi mmoja.
Mkataba wa Curtis Jones unasalia na mwaka mmoja kabla ya kumalizika, jambo ambalo linaongeza imani ya Inter kwamba Liverpool hatimaye watapunguza bei yao ya mauzo.
Kwa mujibu wa Gazzetta, Jones mwenyewe anataka kujiunga na Inter katika dirisha hili la usajili la majira ya joto.
Gazeti hilo pia linaongeza kuwa Nerazzurri wameendelea na mazungumzo na Udinese kuhusu Oumar Solet, na wanalenga kumleta mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26 katika dimba la San Siro kabla ya kuanza kwa maandalizi ya msimu mpya.
Wakati huohuo, Inter wamekaribia kukamilisha usajili wao wa kwanza wa majira ya joto, wakihitimisha mazungumzo na Atalanta kwa ajili ya Marco Palestra katika dili linalozidi thamani ya euro milioni 50.