Jose Mourinho anatarajiwa kuthibitishwa rasmi kuwa kocha mkuu mpya wa Real Madrid baada ya Florentino Pérez kuchaguliwa tena kuwa rais wa klabu hiyo hadi mwaka 2030.

Mourinho, mwenye umri wa miaka 63, alisaini mkataba wa miaka mitatu mwezi uliopita ili kuwa kocha mkuu wa Real Madrid, lakini mkataba wake ulikuwa na masharti kwamba ungeanza kutumika tu ikiwa Pérez angeendelea kushikilia nafasi yake ya urais.
Pérez mwenye umri wa miaka 79, ambaye alipata asilimia 65 ya kura, amekuwa rais wa Real Madrid tangu mwaka 2009 na alitangaza uchaguzi huo katika mkutano maalum na wa dharura na waandishi wa habari mwezi uliopita.
“Tumeshinda uchaguzi na tutaendelea kufanya kazi ili kuendelea kushinda mataji,” alisema Pérez. “Bado niko hapa na niko hapa kuitetea Real Madrid.
“Tutaendelea kufanya kazi ili Real Madrid iendelee kushinda mataji, na tutapambana hadi mwisho ili kutwaa Kombe la Ulaya la 16. Tutaendelea kujivunia Uwanja wa Santiago Bernabéu, ambao ni uwanja bora zaidi duniani.”
“Tunajivunia kuwa na wachezaji bora zaidi duniani, tunajivunia kumkaribisha tena mmoja wa makocha bora zaidi duniani, Madridista wa kweli, Jose Mourinho. Na ninaweza kuwahakikishia kwamba nikiwa rais, Real Madrid imekuwa, ipo na itaendelea kuwa mali ya wanachama wake.”

Real Madrid inamilikiwa kikamilifu na wanachama wake, ambao ndio wanaomchagua rais wa klabu. Huu ulikuwa uchaguzi wa kwanza wa urais ndani ya miaka 20 kuwa na mpinzani, ambaye alikuwa mfanyabiashara mkubwa wa nishati jadidifu, Enrique Riquelme.
Perez alitarajiwa kushinda uchaguzi huo na aliahidi kutoa ofa ya rekodi ya klabu kwa ajili ya kumsajili “mchezaji mkubwa” ambaye hakumtaja jina, iwapo angechaguliwa tena.
Alipata asilimia 100 ya kura zilizohesabiwa kwa njia ya kupiga kura ana kwa ana na kwa posta, akikusanya kura 21,741 dhidi ya kura 11,814 za Riquelme (asilimia 35).
Mourinho anaondoka katika nafasi yake ya kocha wa Benfica, ambapo aliteuliwa mwezi Septemba na kuiongoza timu hiyo kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye Ligi Kuu ya Ureno (Primeira Liga) msimu huu.



