Juventus hawajakata tamaa katika harakati za kumsajili Alexander Sørloth, huku kocha Luciano Spalletti akiendelea kuwa na hamu ya kumleta mshambuliaji huyo wa Atletico Madrid licha ya kuwasili kwa Randal Kolo Muani. Hatma ya dili hilo inaweza pia kutegemea mustakabali wa Nico Gonzalez.

Kwa mujibu wa Tuttosport, Spalletti amekuwa akimvutiwa Sørloth kwa muda mrefu, akimuona kama mshambuliaji wa ndani ya eneo la hatari (target man) anayefaa mfumo wake wa uchezaji. Inadaiwa kuwa kocha huyo aliwasiliana binafsi na nyota huyo wa kimataifa wa Norway ili kumweleza mipango yake.
Mazungumzo na Atletico Madrid yalikuwa tayari yameanza chini ya uongozi wa zamani wa Damien Comolli na Marco Ottolini, huku Sørloth akielezwa kuwa alikuwa na shauku ya kuhamia Turin. Hata hivyo, mabadiliko yaliyotokea katika uongozi wa Juventus, ikiwemo kuondoka kwa Comolli na kuwasili kwa Giovanni Carnevali kama Mtendaji Mkuu (CEO) pamoja na Frederic Massara kama Mkurugenzi wa Michezo, yalisababisha mazungumzo hayo kupungua kasi.
Aidha, tathmini ya Atletico Madrid ya takribani euro milioni 40 kwa mshambuliaji huyo imekuwa kikwazo kingine katika kukamilika kwa uhamisho huo. Hata hivyo, katika siku za hivi karibuni, mazungumzo yamefufuliwa tena kupitia Nico Gonzalez.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Argentina hajaficha nia yake ya kutaka kuungana tena na kocha Diego Simeone, na Atletico Madrid wanaendelea kumfuatilia kwa karibu. Hata hivyo, Juventus wanataka angalau euro milioni 30 kabla ya kukubali kuanza mazungumzo rasmi ya uhamisho.
Juventus wanaweza kukubali kupunguza ada hiyo, lakini kwa sharti moja: Atletico Madrid wakubali kumtoa Alexander Sørloth kwa mkopo wa kulipiwa kuelekea Turin.



