Ripoti kutoka Uingereza zinasema kuwa Manchester United huenda wakamlenga kiungo wa kimataifa wa Italia, Sandro Tonali, ili kuchukua nafasi ya Casemiro anayetarajiwa kuondoka katika eneo la kiungo wakati wa dirisha la usajili wa majira ya kiangazi.

Wakala wa Tonali, Beppe Riso, hivi karibuni amechochea tetesi za usajili baada ya kutoa mahojiano kwa Tuttosport, akidokeza kuwa mteja wake anaweza kuondoka Newcastle siku za usoni.
“Majadiliano ya usajili yatafanyika baadaye. Tutaona msimu utaishaje kisha tuamue nini cha kufanya,” alisema Riso.
Kulikuwepo na ripoti fupi zilizomhusisha Tonali na uhamisho kwenda Arsenal siku ya mwisho ya dirisha la usajili la Januari, lakini kutokana na ada kubwa inayotarajiwa na ugumu wa mazungumzo, hilo halikuwezekana katika masaa ya mwisho ya dirisha. Juventus pia wamekuwa wakimfuatilia kwa muda mrefu kiungo huyo wa zamani wa AC Milan.
Sasa, kulingana na ripoti za The Telegraph, Tonali yuko “juu kabisa” katika orodha ya wachezaji wa kiungo wanaolengwa na Manchester United kwa usajili wa majira ya kiangazi. United wanahitaji kiungo mpya kuchukua nafasi ya Casemiro, ambaye ataondoka klabuni mwishoni mwa msimu wa 2025/26.


