Scott McTominay aliisaidia Napoli kutwaa taji jingine baada ya kuonyesha kiwango cha juu dhidi ya Bologna katika mchezo wa Supercoppa Italiana.

Kiungo huyo wa zamani wa Manchester United alipongezwa kwa nguvu na uwezo wake wa kimichezo kufuatia uchezaji wake bora akiwa na Napoli. McTominay alicheza dakika zote 90 wakati mabingwa wa Italia, wakiongozwa na kocha Antonio Conte, walipopata ushindi wa haki wa mabao 2-0 dhidi ya Bologna katika fainali ya Supercoppa Italiana iliyochezwa Riyadh, Saudi Arabia, Jumatatu.
Winga wa Kibrazili wa Napoli, David Neres, ndiye aliyeng’ara zaidi kwa kufunga mabao yote mawili, moja kabla na lingine baada ya mapumziko ya kipindi cha kwanza.
Hata hivyo, mchango wa McTominay ulionekana wazi na uliendana na hadhi ya tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka wa Serie A aliyonyakua msimu uliopita, kutokana na kiwango chake bora cha ligi na ushiriki wake katika nyakati nyingi nzuri za Napoli.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 alitoa pasi maridadi ya kupenyeza mapema kwa Eljif Elmas iliyomuweka mshambuliaji huyo wa Macedonia katika nafasi nzuri ya kufunga, lakini alikosa kupata asisti baada ya mwenzake kupiga shuti lililopita lango.

McTominay alikaribia pia kujipatia bao muda mfupi kabla ya mapumziko ya kipindi cha kwanza ili kuiongezea Napoli uongozi, lakini alizuiwa na kipa wa Bologna, Federico Ravaglia. Aliendelea kutawala eneo la kiungo kwa uwepo wake wenye nguvu na uimara wa mwili, huku akichangia kwa kiasi kikubwa katika kujenga mashambulizi.
Katika dakika ya 77, alikosa tena bao baada ya jaribio la akrobatiki kwenye nguzo ya mbali, muda mfupi baada ya kuwa na mchango muhimu katika bao la pili la Neres kwa kumweka presha kipa wa Bologna.
Napoli na McTominay watarudi kwenye michuano ya Serie A baada ya Krismasi wakimenyana na Cremonese ya Jamie Vardy, ambapo kwa sasa wapo nyuma kwa pointi mbili dhidi ya vinara wa ligi, Inter Milan.