Marcelo Bielsa mwenye umri wa miaka 67 ambaye alikuwa nje ya usimamizi wa soka tangu alipoondoka Leeds karibu miezi 15 iliyopita, ameteuliwa kuwa kocha mkuu wa Uruguay.

Shirikisho la Soka la Uruguay lilithibitisha kuteuliwa kwa Bielsa kuhusu mkataba utakaodumu hadi Kombe la Dunia la 2026. Anamrithi Diego Alonso kama kocha wa timu ya taifa.
Mkataba wa Alonso ulimalizika baada ya Kombe la Dunia nchini Qatar mwanzoni mwa msimu huu, ambapo Uruguay ilitolewa kwa mshtuko katika hatua ya makundi.
Marcelo aliwahi kuwa meneja wa Argentina kuanzia 1998 hadi 2004 na pia alikuwa na muda wa miaka minne akiinoa Chile.

Kocha huyo aliiongoza Leeds kurejea Ligi Kuu kutoka kwa Ubingwa mwaka 2020 na alikuwa mmoja wa wasimamizi maarufu katika historia ya klabu hiyo. Lakini aliondoka Februari mwaka jana kufuatia kushindwa mara nne mfululizo kwenye ligi.
Maisha yake ya muda mrefu ya usimamizi pia yamejumuisha vipindi vya Athletic Bilbao, Marseille na Lille.
Uruguay kwa sasa wako katika nafasi ya 16 katika viwango vya ubora vya FIFA duniani, huku kampeni ya kwanza kuu ya Bielsa kwenye usukani ikitarajiwa kuwa Copa America mwaka ujao nchini Marekani.

