Thomas Tuchel amesaini mkataba mpya na timu ya taifa ya Uingereza utakaodumu hadi pale michuano ya Euro 2028 itakapofika.

Kocha huyo Mjerumani alichukua mikoba ya kuinoa Three Lions Januari mwaka jana na aliiongoza Uingereza kufuzu Kombe la Dunia 2026 kwa rekodi ya asilimia 100, baada ya kushinda mechi zote nane alizosimamia.
Mkataba wa awali wa Tuchel ulikuwa umepangwa kumalizika baada ya mashindano hayo ya kiangazi, lakini sasa amekubali kuongeza muda wake wa kuinoa timu hiyo kwa miaka miwili zaidi.
“Thomas Tuchel amesaini mkataba mpya wa kuiongoza timu ya wakubwa ya wanaume ya Uingereza hadi UEFA EURO 2028 nchini Uingereza na Ireland,” ilisoma taarifa kwenye tovuti ya Shirikisho la Soka la Uingereza.
Baada ya kuiongoza Three Lions bila kupoteza katika kampeni ya kufuzu iliyovunja rekodi kwa ajili ya Kombe la Dunia lijalo la FIFA litakalofanyika Canada, Mexico na Marekani, Tuchel amekubali kubaki kama kocha mkuu kwa miaka miwili zaidi.
Uingereza hawakufungwa bao hata moja katika kampeni hiyo ya mafanikio, wakifunga mabao 20, na wameendelea kubaki miongoni mwa timu tano bora duniani kwa miaka saba na nusu sasa.


