Liverpool FC na Arsenal FC wako tayari kuingia kwenye ushindani mkali dhidi ya vigogo wa La Liga, Barcelona, katika mbio za kumsajili beki nyota wa Inter Milan, Alessandro Bastoni, kwa mujibu wa CaughtOffside.

Bastoni anatambuliwa kwa upana kama mmoja wa mabeki bora barani Ulaya, akiwa amekulia katika mfumo wa soka na hatimaye kujihakikishia nafasi ya kudumu katika kikosi cha kwanza cha Nerazzurri.
Kwa sasa, Inter wanaongoza ligi wakiwa na tofauti ya pointi 10 dhidi ya wapinzani wao AC Milan katika mbio za kutwaa taji la Scudetto, kuelekea Dabi ya Milan mwishoni mwa wiki. Bastoni amekuwa mhimili muhimu katika harakati zao za ubingwa.
Vinara hao wa Serie A hawapo tayari kumuachia kirahisi mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26, ambaye ana mkataba unaodumu hadi mwaka 2028.
Hata hivyo, Liverpool na Arsenal wanafuatilia kwa karibu hali ya Bastoni nchini Italia iwapo Inter wataamua kusikiliza ofa.

Liverpool wanapima chaguo la mabeki wa kati kabla ya dirisha la majira ya joto, huku mustakabali wa Ibrahima Konate ukiwa shakani. Mkataba wake wa sasa unaisha mwishoni mwa msimu na mazungumzo kati yake na klabu yamekwama.
Tayari Liverpool wamethibitisha usajili wa Jeremy Jacquet kutoka Rennes, lakini bado wanachunguza soko la mabeki wa kati wakitafuta mrithi wa muda mrefu wa nahodha Virgil van Dijk.
Van Dijk amebakiza zaidi ya miezi 12 katika mkataba wa miaka miwili aliotia saini Aprili iliyopita, huku akitarajiwa kutimiza miaka 35 mwezi Julai.
Raia mwenzake Micky van de Ven pia ametajwa kama mrithi anayetarajiwa, huku mustakabali wake katika Tottenham Hotspur ukiwa haujulikani.
Kwa upande wa Arsenal, wanaweza kutoa ushindani mkubwa katika harakati zozote za kumsajili Bastoni. Hata hivyo, klabu hizo mbili za England pamoja na Barcelona watalazimika kutoa takriban pauni milioni 100 ili kuishawishi Inter kumuachia mmoja wa wachezaji wao muhimu.


