Kocha wa muda wa Tottenham, Igor Tudor, amesema ana imani zaidi kuwa timu hiyo itabaki kwenye Premier League licha ya kupoteza nyumbani kwa mabao 3-1 dhidi ya Crystal Palace, matokeo yaliyozidisha presha kwake.

Ushindi wa West Ham United dhidi ya Fulham siku ya Jumatano uliianza saa 24 mbaya kwa klabu hiyo ya kaskazini mwa London. Kipigo hiki cha tano mfululizo kwa Tottenham Hotspur kinamaanisha sasa wako pointi moja tu juu ya eneo la kushuka daraja huku wakiwa na mechi tisa zilizosalia.
Bao la Dominic Solanke katika dakika ya 34 lilionekana kubadilisha mwelekeo wa mchezo kwa Tottenham, lakini nahodha wa muda Micky van de Ven alitolewa kwa kadi nyekundu dakika nne baadaye katika tukio lililoshangaza wengi. Baada ya hapo, Tottenham waliruhusu mabao matatu kabla ya mapumziko ya kipindi cha kwanza.
Mashabiki wengi wa Spurs walianza kuondoka uwanjani wakati wa mapumziko, na ingawa kikosi cha Tudor kilionyesha kupambana katika kipindi cha pili, kipigo hiki kimeifanya timu hiyo kufikisha mechi 11 mfululizo bila ushindi rekodi mbaya zaidi katika historia ya klabu hiyo kwenye EPL.
Igor aliajiriwa mwezi uliopita akitarajiwa kubadilisha mwenendo wa matokeo ya timu, lakini badala yake amekuwa kocha wa kwanza wa Tottenham katika enzi ya EPL kupoteza mechi zake tatu za kwanza. Hivyo alilazimika kujibu maswali kuhusu mustakabali wake baada ya mchezo.


