Szoboszlai amekuwa nyota mkubwa kwa The Reds tangu alipojiunga nao kutoka RB Leipzig mwaka 2023, na kiwango chake akiwa na mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Uingereza kimevutia macho ya Los Blancos.
Nyota huyo mwenye uwezo mkubwa wa kushambulia na kusaidia ulinzi amekuwa mwanga wa matumaini kwa klabu hiyo ya Merseyside licha ya msimu usioridhisha sana chini ya kocha Arne Slot.
Kocha mkuu wa Hungary, Marco Rossi, hivi karibuni alichochea tetesi za uhamisho kwenda Santiago Bernabeu kwa kudai kuwa ‘ndoto’ ya Szoboszlai ni siku moja kuichezea Real Madrid.
“Kwa sababu ya uhusiano wa karibu sana na wa moja kwa moja nilionao na Dominik Szoboszlai tangu alipokuwa mdogo na kuanza kucheza soka, Real Madrid daima imekuwa ndoto yake.Sijui kama ataweza kuchukua hatua hiyo, kwa sababu uamuzi unamtegemea yeye pamoja na klabu yake.” Alisema Rossi.

Hata hivyo, Rossi aliongeza haraka kuwa anaamini nahodha huyo wa Hungary anaweza pia kuongeza mkataba wake Liverpool, akisema: “Siondoi kabisa uwezekano wa yeye kubaki Liverpool na kuongeza mkataba wake huko, hasa kwa sababu anathaminiwa sana ndani ya klabu.”
Inaaminika kuwa The Reds wanajiandaa kumpa ofa mpya ya mkataba mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25, ambaye kwa sasa ana mkataba unaomfunga Anfield hadi mwaka 2028.
Wakati huo huo, Real Madrid wanatarajiwa kuimarisha safu yao ya kiungo msimu huu wa joto, huku chipukizi wa AZ Alkmaar, Kees Smit, akitajwa kuwa miongoni mwa malengo ya klabu hiyo ya Hispania.
Kijana huyo aliwahi kuhusishwa na uhamisho kwenda Newcastle mwezi Januari, huku Liverpool pia wakiripotiwa kufuatilia kwa karibu maendeleo ya nyota huyo wa Uholanzi.