Kipa wa Atletico Madrid Jan Oblak hakukumbuka kilichotokea na atawekwa chini ya uangalizi baada ya “kuchanganyikiwa kidogo” katika ushindi wa 1-0 wa hapo jana kwenye LaLiga dhidi ya Athletic Bilbao.

Oblak alitolewa nje katika dakika ya 69 kama sehemu ya mabadiliko matatu kutokana na tatizo la bega, huku mbadala wake Ivo Grbic akiokoa dakika za mwisho huko San Mames.
Atletico walithibitisha hilo baada ya mchezo huo kwamba mlinda mlango huyo wa Slovakia alitolewa kwa sababu alikuwa amechanganyikiwa kidogo, pia alipata majeraha ya moja kwa moja kwenye bega lake la kulia.
Kocha mkuu wa Atletico Diego Simeone aliongeza kwa kusema kuwa; “Jan hakukumbuka mengi ya kilichotokea sijazungumza naye, lakini daktari aliniambia kuwa hakumbuki.”
Klabu hiyo ilisema Oblak alifanyiwa uchunguzi wa mishipa ya fahamu baada ya mchezo bila dalili zozote za wasiwasi, lakini atawekwa chini ya uangalizi wa madaktari. Oblak alijaribu kucheza baada ya kuonekana akiuguza jeraha la bega kabla ya kuzimia katika dakika ya 69.

Mlinda mlango huyo ameanza mechi nane kati ya tisa za ligi ya Atletico msimu huu, baada ya kusumbuliwa na tatizo la paja mapema Septemba.

