Wilfried Zaha anaripotiwa kufanya mazungumzo na Paris Saint-Germain juu ya uhamisho wa bure msimu huu wa joto.

Nyota huyo wa Crystal Palace anaonekana kukaribia kuondoka Selhurst Park mkataba wake utakapomalizika mwishoni mwa mwezi huu lakini bado hajathibitisha ni wapi ataelekea.
Zaha mwenye miaka 30, anadaiwa kupewa ofa ya kuhamia Saudi Arabia katika wiki za hivi karibuni, jambo ambalo lingemfanya kuwafuata Karim Benzema na Cristiano Ronaldo kwenda Mashariki ya Kati.
Lakini gazeti la The Sun linaonyesha raia huyo wa Ivory Coast sasa yuko kwenye mazungumzo ya kubaki Ulaya kwa kuhamia miamba ya Ligue 1 PSG.

Ingawa hakuna ofa madhubuti kutoka kwa WaParisi kwa wakati huu, kuhamia mji mkuu wa Ufaransa bila shaka kutamfaa Zaha kwa kuwa hakuficha nia yake ya kucheza soka ya Ligi ya Mabingwa.
Palace wanataka nyota wao kusalia na wametoa kandarasi ya pauni 200,000 kwa wiki ili kumbakisha London Kusini.

Pia kuna nia nyingine ya Ulaya ya kuzingatia, huku AC Milan ikisemekana kuwa miongoni mwa vilabu vinavyoshinikiza kumnasa Zaha bila malipo.

