Usajili mpya wa Milan, Niclas Fullkrug, anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa mara nyingine, baada ya mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Ujerumani kuripotiwa kuvunjika kidole cha mguu baada ya kucheza dakika 106 pekee kwenye Serie A.

Fullkrug alikuwa mchezaji wa kwanza mpya kuwasili kwenye dirisha la usajili la Januari la Serie A alipokamilisha uhamisho wa mkopo kwenda Milan akitokea West Ham United, ikiwa na kipengele cha kununuliwa, tarehe 2 Januari.
Mshambuliaji huyo wa Ujerumani alikuwa tayari akifanya mazoezi na Rossoneri kwa wiki moja kabla ya kukamilisha dili hilo, alitambulishwa rasmi Januari 2, kisha akacheza mechi yake ya kwanza ya Serie A jioni hiyo hiyo katika ushindi wa ugenini wa 1-0 dhidi ya Cagliari.
Baada ya hapo, aliingia kama mchezaji wa akiba kwa mechi ya pili mfululizo katika sare ya 1-1 dhidi ya Genoa pale San Siro, kabla ya kuanza kikosi cha kwanza kwenye sare ya 1-1 dhidi ya Fiorentina siku ya Jumapili.

Hata hivyo, kwa mujibu wa ripoti kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini Italia, Fullkrug alivunjika kidole cha mguu kuelekea mwisho wa mechi yake ya kwanza kamili akiwa na jezi ya Milan dhidi ya Fiorentina, na sasa anakabiliwa na kipindi cha kuwa nje ya uwanja baada ya kucheza dakika 106 pekee za Serie A.
Bado haijafahamika ni kwa muda gani mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 32 atakuwa nje ya uwanja, lakini anatarajiwa kukosa mchezo wa Alhamisi wa Serie A ugenini dhidi ya Como.
Awali, Sky Sport Italia iliripoti kuwa Fullkrug angekuwa nje kwa wiki kadhaa, lakini sasa inaeleza kuwa jeraha hilo si baya kama ilivyodhaniwa mwanzoni, na kwamba atajaribu kurejea kwa wakati ili kuikabili Lecce siku ya Jumapili. Milannews.it inadai kuwa mchezaji huyo wa Ujerumani ana uwezekano mkubwa wa kukosa mechi ya mwishoni mwa wiki.


