Ruben Loftus-Cheek alilazimika kutolewa uwanjani kwa machela baada ya kupata pigo usoni wakati wa kipigo cha AC Milan dhidi ya Parma jana.

Kiungo huyo wa kimataifa wa Uingereza anatarajiwa kufanyiwa upasuaji baada ya kuvunjika taya katika mechi hiyo ya Serie A. Ruben Loftus-Cheek alitolewa katika dimba la San Siro takribani dakika ya 10 kufuatia kugongana na kipa wa Parma, Edoardo Corvi, alipokuwa akijaribu kuunganisha krosi. Milan walipoteza mechi hiyo kwa mabao 1-0.
Vyombo vya habari vya Italia viliripoti ukubwa wa jeraha hilo, huku Sky Sports Italia ikisema: “Mbali na kuvunjika meno ya juu na kupata michubuko miwili, Muingereza huyo alipata pia ufa kwenye mfupa wa alveolar.”
Ripoti hiyo iliongeza kuwa Loftus-Cheek “atafanyiwa upasuaji Jumatatu… na anatarajiwa kuwa nje kwa miezi kadhaa.”
Sasa Loftus-Cheek anaonekana kukabiliwa na kipindi kirefu nje ya uwanja, jambo linaloweka ndoto zake za kushiriki FIFA World Cup ya majira ya joto katika hatari kubwa.
Mashindano hayo yanaanza ndani ya miezi isiyozidi minne, na ni vigumu kwa Ruben Loftus-Cheek kucheza mechi nyingi kabla ya hapo huku akiendelea kupona baada ya upasuaji wa taya.


