Huu utakuwa mchezo muhimu kwa Real Madrid ambao tayari wameondolewa kwenye Copa del Rey na pia wakiwa nyuma kwa pointi nne dhidi ya Barcelona wanaoongoza msimamo wa ligi.
Mbali na hilo, klabu hiyo pia inakabiliwa na majeraha kadhaa ya wachezaji, huku Kylian Mbappe akiwa bado anarejea baada ya kupata maumivu, wakati Rodrygo anaweza kuukosa msimu mzima kutokana na jeraha la muda mrefu.
Kutokana na wimbi hili la majeraha, hasa lile linalomhusu Mbappe, Real Madrid wanamtegemea sana Vinicius Jr. kuelekea katika pambano hili dhidi ya Manchester City.
Kwa mujibu wa gazeti la AS, mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Brazil anatarajiwa kuwa mtu muhimu zaidi kwa Real Madrid watakapokutana na vigogo hao wa Ligi Kuu ya Uingereza.
Ingawa kwa kiasi fulani ameonekana kuwa nyuma ya Mbappe msimu huu, Vinicius hajafanya vibaya sana kwani amehusika katika mabao 24 kwenye mashindano yote.

Aidha, kiwango chake cha hivi karibuni kinatia matumaini, hasa baada ya kuhusika katika mabao sita ndani ya michezo minne iliyopita ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Kuhusu rekodi yake dhidi ya Manchester City, Vinicius amekutana nao mara kumi, akishinda michezo minne na kutoka sare miwili.
Mshambuliaji huyo wa Brazil amefunga mabao mawili pekee dhidi ya kikosi cha Pep Guardiola, lakini pia ametoa pasi tano za mabao katika michezo hiyo kumi.
Kwa upande wa Real Madrid, klabu hiyo ina imani kubwa kwa Vinicius Jr., na inaamini kwamba mshambuliaji huyo atalazimika kuonyesha kiwango cha juu ikiwa Los Blancos wanataka kupata matokeo mazuri katika mchezo wa kwanza wa mchujo huu.