Bayern Munich hawana uwezo wa kifedha wa kumsajili Phil Foden kutoka Manchester City.

Baada ya ripoti kwamba Bayern wanamuwinda Foden, mchambuzi Christian Falk aliiambia SportBild kuwa mchezaji huyo ni ghali sana kwa klabu hiyo ya Bundesliga.
Ripoti za awali zilidai kuwa kocha Vincent Kompany anamkubali sana kiungo huyo mshambuliaji na angependa kumuona akijiunga na Bayern.
Hata hivyo, imeelezwa pia kuwa Manchester City hawana mpango wa kumuuza mchezaji huyo wa kimataifa wa Uingereza, na licha ya kukosa nafasi ya kucheza mara kwa mara kwa sasa, Foden anataka kubaki kwenye klabu yake ya utotoni.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 ameichezea Manchester City maisha yake yote ya soka la kulipwa, akicheza mechi 360 tangu atoke kwenye akademi, na ingawa mara kadhaa ameanza kutoka benchi msimu huu, bado anaendelea kuwa na dhamira ya kubaki Etihad.
Ripoti nyingine kutoka kwa Falk inaonyesha kuwa nafasi ya Bayern kumsajili ni ndogo zaidi, kwani hawahitaji mchezaji wa aina yake na pia wanamuona kuwa ghali kupita uwezo wao.

Falk alisema: “Phil Foden ni jina ambalo lingeamsha shauku kubwa kwa mashabiki wa Bayern, lakini ukweli ni kwamba klabu haitafuti mchezaji wa aina hiyo. Thamani yake ya soko ya euro milioni 80 ipo juu ya bajeti ya mkurugenzi wa michezo Max Eberl kwa mchezaji wa kushambulia.”
Klabu inataka mchezaji wa akiba kwa upande wa kushoto badala ya mchezaji anayetarajia kuwa chaguo la kwanza. Nafasi nyingine zote anazocheza tayari zimejaa wachezaji wa kiwango cha juu Bayern. Katikati wameongeza mkataba wa Serge Gnabry, anayeziba nafasi ya Jamal Musiala.
“Kulia, Bayern wana Michael Olise, ambaye huenda ndiye winga bora barani Ulaya kwa sasa. Pia yupo Lennart Karl mwenye mustakabali mzuri. Hivyo kwa sasa, Foden si chaguo kwa Bayern.”
Inaelezwa kuwa mazungumzo ya mkataba mpya kati ya Manchester City na Foden yanaendelea vizuri, huku klabu hiyo inayoshika nafasi ya pili kwenye EPL ikiwa haina mpango wa kumuachia nyota wao.
Hii ina maana kuwa hakuna nia ya kusikiliza ofa kutoka klabu nyingine barani Ulaya, hata kama zipo zinazoweza kumudu gharama yake.


