Gary Lineker amedai kuwa Julian Alvarez hafurahishwi na hali yake ndani ya klabu ya Atletico Madrid, huku akihusishwa na uwezekano wa kujiunga na Arsenal.

Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Argentina anaripotiwa kuwa kwenye rada ya The Gunners kuelekea dirisha la usajili la majira ya kiangazi, wakati Mikel Arteta akitafuta kuimarisha zaidi safu yake ya ushambuliaji.
Arsenal, ambao wamekosolewa na Jamie Carragher kwa kukosa ubora katika eneo la ushambuliaji, wameshuhudia mabao yakipungua kutoka kwa washambuliaji wao wa sasa katika wiki za karibuni, hali ambayo imeathiri pia azma yao ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza.
Kwa upande mwingine, Alvarez amefunga mabao 11 katika mechi 29 alizocheza kwenye mashindano yote akiwa na Atletico, ingawa ameshindwa kufunga katika kila moja ya mechi zake kumi za mwisho za LaLiga.
Kwa mujibu wa ripoti mbalimbali, Atletico wanaweza kuwa tayari kumuuza mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 mwishoni mwa msimu kwa ada inayokadiriwa kufikia pauni milioni 86.
Katika kile kinachoonekana kuwa habari njema kwa Arsenal, Lineker ametoa taarifa ambayo inaweza kuwapa mashabiki matumaini juu ya uwezekano wa dili hilo kutimia.


