Beki wa Inter, Benjamin Pavard, asisitiza kuwa ‘alihitaji’ kujifunza aina mpya ya soka alipojiunga na Nerazzurri mwaka 2023, na anaona hamu ya ‘kulipiza kisasi’ kwa wachezaji wenzake waliopoteza Fainali ya Ligi ya Mabingwa mwaka 2023.

Pavard alizungumza na gazeti la Kifaransa L’Équipe siku tatu kabla ya Fainali inayosubiriwa kwa hamu ya Ligi ya Mabingwa ya mwaka 2025 kati ya Inter na PSG mjini Munich.
“PSG ni timu kubwa. Wamekuwa wakilionesha hilo kwa miaka mingi, na nafikiri sasa wako thabiti zaidi. Ni kikosi imara chenye kocha bora — mmoja wa bora duniani. Wanacheza soka safi, ni furaha kuwaangalia, lakini Jumamosi hatutakuwa watazamaji.” alisema beki huyo wa Kifaransa kupitia Gazzetta.
Pavard tayari alishawahi kushinda Ligi ya Mabingwa akiwa na Bayern Munich, walipoifunga PSG kwenye fainali mwaka 2020, ingawa hakushiriki mechi hiyo kutokana na jeraha.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa alikosa nusu fainali kali dhidi ya Barcelona hivi karibuni, lakini anatarajiwa kurejea dimbani kwa fainali hiyo ya Jumamosi.

“Kutakuwa na nyakati ngumu, lakini siogopi. Tuna wachezaji wenye uzoefu waliowahi kupitia hali kama hii. Wengi wao wanataka kulipiza kisasi baada ya ile fainali tuliyopoteza dhidi ya Manchester City. Kichapo kile kiliwafundisha mengi — sasa wamekuwa na nguvu zaidi.”
“Tunaweza kufanya kitu cha kipekee. Sio wakati wa kufikiria hilo sasa, lakini kwa baadhi yetu hii inaweza kuwa nafasi ya mwisho ya mafanikio makubwa. Tayari najivunia tulichofanikisha kama timu, na najivunia taaluma yangu pia. Nimefurahi kuwa sehemu ya kikosi hiki.”
Pavard hakuwa sehemu ya kikosi cha Inter walipopoteza fainali ya Ligi ya Mabingwa mwaka 2023, kwani alijiunga na timu hiyo miezi michache baadaye.
“Sisi si kikosi cha nyota wa soka, lakini tunajua kufanya kila kitu pamoja. Tunajua jinsi ya kustahimili vizingiti pamoja. Kama inahitajika kurudi nyuma na kujilinda, tunajua kufanya hivyo,” aliongeza.
Pavard alisema kuwa wanaweza kushambulia kwa presha ya juu, lakini pia wakakaa chini kujilinda. Hawabadilishi mbinu mara moja, lakini wakiona hawawezi kuupora mpira mbele, wanarudi kwenye safu ya kati. Jambo la muhimu zaidi ni kutoruhusu bao. Wakati mwingine lazima urudi nyuma na ustahimili ili kushinda.


