Baada ya kupoteza mchezo wa hatua ya robo fainali ya kwanza Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Al Masry, uongozi wa Simba umebainisha kuwa sababu iliyowafanya washindwe kupata ushindi ni kukwama kutumia nafasi ambazo walizipata kwenye mchezo huo.
Simba chini ya Kocha Mkuu, Fadlu Davids, Aprili 2 2025 baada ya dakika 90 walishuhudia ubao wa Uwanja wa Suez Canal ukisoma Al Masry 2-0 Simba ambapo kwenye eneo la ushambuliaji Fadlu alianza na Leonel Ateba.
Mabao kwenye mchezo huo yalifungwa kila moja kipindi chake, ambapo kipindi cha kwanza ni Abderrarhim Deghmoum alianza kupachika bao la uongozi dakika ya 15 kwa shuti kali akiwa nje ya 18 likimshinda Moussa Camara.
Kipindi cha pili ilipachikwa kamba ya pili ambayo ni mali ya John Okoyo dakika ya 89. Mfungaji wa bao la pili alianzia benchi kwenye mchezo huo alipoingia alipachika bao hilo akiwa ndani ya 18.
Murtaza Mangungu, Mwenyekiti wa Simba amebainisha kuwa walikuwa na uwezo wakupata matokeo ugenini jambo ambalo lilishindikana kutokana na nafazi walizotengeneza kushindwa kutumiwa.
“Tulikuwa na nafasi yakupata matokeo kwenye mchezo wetu hilo halikuwezekana kwa kuwa nafasi tulizopata hatukufunga, bado ni mchezo wa kwanza upo mchezo wa pili Uwanja wa Mkapa tunaamini tutapambana kupata matokeo ili kutinga hatua ya nusu fainali.”
Miongoni mwa nafasi ambazo walizitengeneza Simba ni kupitia kona zilizopigwa na Ellie Mpanzu alifanya hivyo dakika ya 14, 39, 43, 57 na 86 hazikuwa na faida kwa Simba na alichezewa faulo dakika ya 37 na Ahmed Aid ambaye alionyeshwa kadi ya njano.