Rais wa klabu ya Barcelona Joan Laporta amesema kuwa kwasasa wanapaswa kutazama mbele na walijua kuwa katika mchakato huo wa kuijenga timu upya timu kutakuwa na kupanda na kushuka.

Laporta ameyasema hayo jana, baada ya timu yake kucharazwa wakiwa nyumbani kwa mabao 3-0 dhidi ya Bayern Munich kwenye michuano ya Klabu Bingwa barani Ulaya ambapo kupoteza kwao kumewafanya waende kushiriki michuano ya Uropa Ligi.
Mechi ya jana mpaka inamalizika vijana wa Xavi Hernandez walishindwa hata kupiga shuti ambalo limelenga lango huku Bayern wakipiga mashuti 7 ambayo yalilenga lango. Mechi ya kwanza Barcelona walikufa kwa mabao 2-0, huku matarajio yao yakiwa kulipiza kwenye mechi ya marudiano.
Barca ambaye alikuwa katika kundi C, ataenda kushiriki Europa huku ikiwa ni kwa mara ya pili mfululizo kushindwa kuingia hatua ya 16 bora huku waliofuzu hatua inayofuata ni Bayern Munich na Intermilan, wakati kwa upande wa Viktoria Plzen yeye akitolewa moja kwa moja kwani hajashinda mchezo wowote .

Msimu uliopita alipoingia michuano ya Europa Ligi alitolewa katika hatua ya Robo Fainali dhidi ya Eintracht Frankfurt ambao ndio walibeba kombe hilo huku Barca akiondoka patupu.
Laporta ametoa ujumbe kwa mashabiki wa Barca na kuwaambia kuwa kwa muda huu waangalie mbele mechi zinazokuja huku kocha wa timu hiyo Xavi akiwafanya vijana wacheze ili wakue kwa kiwango kinachohitajika.


