Casemiro: Ningependa kucheza na Cristiano Ronaldo.

Kiungo mpya wa Manchester United Casemiro amemsihi Cristiano Ronaldo kusalia Manchester United kabla ya kuhamia Old Trafford ili waweze kucheza pamoja. Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 30 amejiunga na United kwa paundi milioni 70 kutoka Real Madrid na anatarajiwa kutambulishwa kabla ya pambano lao na Liverpool leo usiku.

Casemiro alicheza pamoja na Ronaldo wakati wakiwa Madrid na ana matumaini ya kuungana tena na staa huyo ambaye alishinda naye mataji kadhaa, yakiwemo mataji manne ya Ligi ya Mabingwa.

Ronaldo

Mbrazil huyo aliiaga Real Madrid kwa hisia kali wakati wa mkutano na waandishi wa habari Jumatatu asubuhi na aliulizwa kuhusu hali ya Ronaldo huko United.

Alimsifu nyota huyo wa Ureno, akisema: ’’Sijazungumza na Cristiano, natumai atasalia kwa sababu ni mmoja wa wachezaji bora zaidi wakati wote’’.

”Nataka kuleta maadili yangu kwa Manchester United, kila kitu ambacho Real Madrid ilinifundisha, kushinda siku hadi siku, kutoka kwa kila kipindi cha mazoezi. Ninataka kupata uzoefu wa  kutoka ndani. Ninafurahia kila kitu nilicho nacho’’. Alisema Casemiro.

Ronaldo aliiambia klabu kuwa anataka kuondoka mapema msimu huu wa joto na alikosa muda mwingi wa maandalizi ya msimu mpya, akitamani kuondoka Old Trafford kwenda timu itakayoshiriki Ligi ya Mabingwa.

Lakini timu kama Chelsea, Bayern Munich na Atletico Madrid wamekataa nafasi ya kumsajili na sasa anaweza kusalia Manchester.

Wakati huohuo, Casemiro aliwajibu wale wanaodai kuwa anahamia Old Trafford kwa ajili ya kujinufaisha kifedha, akisisitiza anahisi muda wake wa kukaa Madrid umekwisha kufuatia ushindi wao wa Ligi ya Mabingwa mwezi Mei.

”Wale wanaofikiri ninaondoka kwa ajili ya pesa ni kwa sababu hawanijui, Nadhani ni wachache na hawanijui, sio kwa pesa, wamekosea, sio hivyo’’ alisema.

Kiungo huyo wa kati wa Brazil anatarajiwa kuwa mmoja wa wachezaji wanaolipwa fedha nyingi zaidi United huku akiripotiwa kuwa na mkataba wa pauni 375,000 kwa wiki, pamoja na David De Gea.

”Mwisho wa fainali ya Ligi ya Mabingwa nilihisi mzunguko wangu umekwisha. Mimi ni mkweli. Baada ya likizo, hisia ilikuwa sawa, haikuwa haraka hivyo, Tayari nilizungumza na klabu mara tu ilipomaliza Ligi ya Mabingwa”.

”Mke wangu aliniunga mkono tangu mwanzo, familia yangu daima ilikuwa upande wangu katika uamuzi huu, Ilikuwa vigumu sana kuzungumza na rais, lakini siku zote alikuwa mkweli kwake.’’Alimaliza kuzungumza Casemiro.

Acha ujumbe