Marcus Rashford amekubali mkataba wa miaka mitatu na Barcelona huku vigogo hao wa La Liga wakijiandaa kufanya uhamisho wake wa mkopo kuwa wa kudumu, kwa mujibu wa chapisho la Hispania la Sport.

Marcus Rashford alihamia kwa mkopo kwa mabingwa hao wa Hispania majira ya joto yaliyopita, akiwa na kipengele cha kufanya uhamisho huo kuwa wa kudumu, baada ya kupoteza nafasi yake kikosini chini ya aliyekuwa kocha wa Manchester United, Ruben Amorim.
Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa England alikuwa na kipindi kizuri kwa mkopo katika Aston Villa katika nusu ya pili ya msimu wa 2024-25, jambo lililoisukuma Barcelona kuonyesha nia ya kumsajili.
Licha ya tetesi kuwa kocha mpya wa United, Michael Carrick, angeweza kufikiria kumrudisha mchezaji huyo wa miaka 28 Old Trafford, Rashford anatarajiwa kusaini rasmi mkataba katika dimba la Spotify Camp Nou, hatua ambayo itamfanya akubali kupunguza mshahara wake kwa kiasi kikubwa.
Barcelona walilipa United pauni milioni 5 za ziada majira ya joto yaliyopita ili kujumuisha kipengele cha pauni milioni 26 cha kumnunua mshambuliaji huyo mwishoni mwa msimu wa 2025-26.


