Paris Saint-Germain, Real Madrid na Inter Milan zote zilikuwa zikimfuatilia beki wa kati wa Liverpool Ibrahima Konate.

Ibrahima Konaté yuko karibu kuongeza muda wa kukaa kwake Liverpool. Liverpool wanakaribia kufikia makubaliano ya mkataba mpya na beki wao nyota Ibrahima Konate, kulingana na mtaalamu wa masuala ya usajili Fabrizio Romano.
Mkataba wa sasa wa Mfaransa huyo unatarajiwa kuisha majira haya ya joto, na kulikuwa na hofu kubwa kwamba angeondoka bure mwishoni mwa mwaka huu.
Mabingwa wa Ligue 1 PSG, wababe wa La Liga Real Madrid na vinara wa Serie A Inter Milan wote walihusishwa na nia ya kumsajili mchezaji huyo wa zamani wa RB Leipzig kwa uhamisho wa bure.
Hata hivyo, timu hizo pamoja na nyingine zinatarajiwa kukosa huduma zake, kwani sasa Konate yuko karibu kukubaliana masharti mapya na Liverpool.
Liverpool wamekuwa wakitamani sana kumuongezea mkataba Konate, lakini mazungumzo yalikuwa yamesimama katika miezi ya hivi karibuni.

Baada ya kufikia hatua kubwa katika mazungumzo, sasa Konate anaonekana yuko tayari kusaini mkataba mpya na mabingwa watetezi wa EPL.
Romano alisema: “Mazungumzo haya yanaelekea katika hatua za mwisho. Makubaliano kati ya Konate na Liverpool yanakaribia sana, yako karibu kukamilika. Bado hayajakamilika rasmi, na tunapaswa kusubiri hadi mwisho kabisa kabla ya kusema yamekamilika, kwa sababu kwa wachezaji huru na muhimu kama Konate, mambo yanaweza kubadilika kwa haraka.”
Lakini kwa sasa, mazungumzo yanaendelea vizuri sana ili kufanikisha mkataba mpya.
Mshahara karibu umekubaliwa, muda wa mkataba bado unajadiliwa, na kuna baadhi ya vipengele vinavyohitaji kufafanuliwa, lakini pande zote mbili ziko karibu sana kufikia makubaliano.
Habari hizi zitakuwa faraja kwa Liverpool, ambao wamekuwa na msimu wa pili usioridhisha chini ya kocha Arne Slot.


