Klabu ya Yanga imefanikiwa kupiga hatua moja mbele katika ligi ya mabingwa Afrika baada ya kupata ushindi wa mabao mawili kwa bila dhidi ya klabu ya El Merreikh nchini Rwanda.
Yanga ni kama imefanikiwa kuona mwanga kuelekea hatua ya makundi barani Afrika baada ya miaka mingi, Kwani imefanikiwa kupata alama tatu muhimu leo dhidi ya El Merreikh wakiwa ugenini.
Wananchi walianza mchezo huo wakionekana wanahitaji alama tatu muhimu kutokana na aina ya mpira waliokua wanaucheza katika kipindi cha kwanza ambapo walionekana kutawala mchezo dhidi ya wenyeji wao.
Mchezo ulimalizika kipindi cha kwanza kwa sare ya bila kufungana lakini kipindi cha pili Wananchi waliongeza kasi na ufanisi mbele ya lango na kufanikiwa kupata mabao mawili kupitia kwa Kenedy Musonda na bao la pili likipachikwa na Clement Mzize.
Yanga sasa wanaweza kuandika rekodi ya kuingia makundi ya ligi ya mabingwa Afrika baada ya kukaa kwa muda mrefu sana, Kwani kushinda mabao mawili kwa bila wakiwa katika kiwanja cha ugenini ni dalili nzuri kuelekea kuandika rekodi.

