Timu ya TP Mazembe imemtimua Kocha wake Franck Dumas, baada ya kushindwa kufuzu hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika hapo jana.

Mazembe imeondolewa hapo jana na Vipers ya nchini Uganda kwa mikwaju ya Penati mbili kwa nne baada ya michezo yote miwili kutoka sare ya bila kufungana. Hivyo basi moja kwa moja itaenda kucheza Kombe la shirikisho.
Saa chache baadae, klabu hiyo ilitoa taarifa kwa vyombo vya habari, inayosema Rais wake Moise Katumbi na Kocha huyo wamefika uamuzi wa kuachana kirafiki baada ya kushindwa kufikia malengo ya timu yao.

Dumas ambaye aliteuliwa July 2021 kuwa Kocha mkuu wa klabu hiyo ya Congo amekuwa akikosolewa kwa mwenendo wake mbaya hasa kwenye michuano ya Afrika.

