KOCHA Mkuu wa klabu ya Yanga Miguel Gamondi amesema hana shinikizo lolote kuelekea msimu ujao na anaimani yakufanya vizuri akiwa na mabingwa hao wa soka la Tanzania.
Miguel amezungumza hayo kwa mara ya kwanza baada ya kuwa kambini kwa siku kadhaa na kutazama kikosi chake kinavyofanya maandalizi.Kwa mujibu wa Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe alisema, kocha huyo raia wa Argentina amesema kwa muda mchache aliokaa na kikosi chake amewaona wachezaji wanaojituma na kujitambua kitu ambacho kinampa imani ya kufanya vizuri na timu hiyo na hana wasiwasi wowote.
“Kocha wetu amesema wazi kuwa kila kitu kipo sawa na amezoea kufanya kazi katika shinikizo hasa katika soka la Afrika, mashabiki wanahitaji matokeo muda wote kwa hiyo ni lazima ukiwa kocha ujue kuishi katika nyakati zote ukiwa umeshinda au umepoteza.“Kocha wetu Miguel amesema anaheshimu kile kilichofanywa na watangulizi wake na anatamani kufanya zaidi ya walipoishia ndio maana ameanza mapema kukisuka kikosi chetum,” alisema.
Gamondi anatarajia kuanza kazi yake ya kwanza kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Kaizer Chiefs kwenye mechi ya kunogesha kilele cha Siku ya Mwananchi kesho Jumamosi kwenye Uwanja wa Benjamini Mkapa, Dar.