Nahodha wa klabu ya Liverpool Jordan Henderson atatimka ndani ya klabu hiyo baada ya kuitumikia kwa muda mrefu na anadaiwa kutimkia Uarabuni msimu ujao.
Henderson amekua kwenye kiwango kikubwa kwa muda mrefu ndani ya klabu ya Liverpool tangu ajiiunge na timu hiyo akitokea Sunderland lakini kiungo ataondoka klabu hiyo na kujiunga na klabu ya Al-Ittihad ya nchini Saudia Arabia.
Kiungo huyo gwiji wa Liverpool amekubaliana maslahi binafsi na klabu ya Al-Ittihad ambapo anatarajiwa kusaini kandarai ili kuweza kutambulishwa kama mchezaji mpya wa klabu hiyo siku kadhaa zijazo.
Henderson ameitumikia klabu ya Liverpool kwa mafanikio makubwa huku akiwa nahodha ambaye ameshinda kila taji ambalo alilipambania ndani ya jezi za klabu hiyo, Kwani ameshinda taji la ligi kuu ya Uingereza, Ligi ya mabingwa ulaya, Klabu bingwa ya dunia, Uefa Super Cup, Fa Cup, pamoja na Carabao Cup.
Liverpool wanatajwa kuingia sokoni kutafuta mbadala wa kiungo Jordan Henderson baada ya kujua mchezaji huyo anatimka klabuni hapo, Huku jina la kiungo wa Southampton Romeo Lavia likiwa kwenye orodha ya juu kabisa.

