Kocha mkuu wa Aston Villa Steven Gerrard ametimuliwa hapo jana na timu yake hiyo baada ya kuwa na mwendelezo mbaya wa matokeo, na kupoteza mchezo dhidi ya Fulham kwa 3-0.

Gerrad mwenye umri wa miaka 42, ameshinda mechi mbili pekee katika michezo 11 waliyocheza kwenye ligi msimu huu, huku kipigo cha kuamkia leo kwenye uwanja wa Craven Cottage, ambacho kilifuatia kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Chelsea mwishoni mwa wiki iliyopita kiliweka hatiani kibarua chake.
Msemaji wa Villa alitoa kauli fupi aliyosema kuwa;“Tungependa kumshukuru Steven kwa bidii na kujitolea kwake na tunamtakia heri kwa siku zijazo.”
Mabao ya Fulham yalitupiwa kimyani na Harrison Reed, Mitrovic pamoja na bao la kujifunga kutoka kwa beki wa Villa Tyrone Mings huku vijana wa Steven Gerrad wakipata adhabu ya kadi nyekundu dakika ya 62.

Kupoteza mchezo wa jana kwa Villa kunawafanya wazidi kuporomoka wakiwa katika nafasi ya 17, michezo ya kupoteza 6 huku wakiwa na pointi 9 kibindoni ambazo sio salama kabisa na kama wakiendelea hivyo hali itazidi kuwa mbaya zaidi.

