Kiungo wa klabu ya Liverpool na timu ya taifa ya Brazil Fabinho taarifa zinaeleza yuko mbioni kuelekea nchini Saudia Arabia kujiunga na klabu ya Al-Ittihad.
Klabu ya Liverpool na Al-Ittihad zinafanya mazungumzo ya dili la Fabinho na namna gani timu hiyo kutoka Saudia watawalipa Majogoo ili kufanikiwa kumbeba kiungo huyo wa ulinzi ambaye ameitumikia klabu hiyo kwa misimu ya kutosha.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Brazil mpaka sasa inaelezwa ameshakubaliana maslahi binafsi na klabu ya Al-Ittihad huku ambacho kinasubiriwa mpaka sasa ni makubaliano baina ya vilabu ili kiungo huyo atimke klabuni hapo.
Fabinho yuko tayari kutimka ndani ya Liverpool baada ya kucheza kwa mafanikio makubwa ndani ya viunga vya Anfield akitokea Monaco mwaka 2017 na anaona huu ni muda sahihi wa yeye kwenda kutafuta changamoto nyingine.
Liverpool mpaka sasa inaonekana kupitisha fagio kwa wachezaji wake waliotumika kwa muda ndani ya timu hiyo ambapo walianza na kiungo James Milner, akafata nahodha Jordan Henderson, na sasa wanakaribia kuachana na kiungo Fabinho ambapo wakati huohuo wako sokoni kutafuta mibadala ya wachezaji hao.

