Winga wa klabu ya Manchester City na timu ya taifa ya Algeria Riyad Mahrez amefanikiwa kufikia makubaliano na klabu ya Al Ahli kwajili ya kujiunga na timu hiyo.
Manchester City watapokea kiasi cha Euro milioni 30 na nyongeza ya Euro milioni 5 ambapo Mahrez mwenye umri wa miaka 32 atafanya vipimo vya afya mapema kesho kwajili ya kusaini mkataba wa miaka mitatu na klabu hiyo.
Winga huyo alishakubaliana maslahi binafsi na klabu ya Al Ahli wiki kadhaa zilizopita kilichokua kinasubiriwa ni kuona klabu ya Al Ahli inapeleka ofa mezani kwa Man City na ndio leo rasmi wamefanikiwa kufikisha ofa hiyo mezani na kukubalika.
Riyad Mahrez anaondoka klabu ya Manchester City akifanikiwa kushinda kila taji ambalo ameshindania na klabu hiyo kwani ameshinda mataji manne ya ligi kuu ya Uingereza akiwa na City huku akishinda moja na Leicester City, kombe la FA, kombe la Carabao, pamoja na taji la ligi ya mabingwa ulaya.
Klabu ya Manchester City kwenye dirisha hili imeachana na wachezaji wake wengi huku Riyad Mahrez akiwa miongoni mwao ambapo Gundogan ndio alifungua milango, Huku wachezaji kama Kylie Walker na Bernardo Silva wakitajwa kuondoka klabuni hapo.

