Bayern Munich waliizamisha Real Madrid kwa mabao ya dakika za mwisho na kufuzu nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa.

Mabao ya kuchelewa kutoka kwa Luis Diaz na Michael Olise yaliihakikishia Bayern ushindi wa kusisimua wa 4-3 dhidi ya Real Madrid Jumatano, wakishinda kwa jumla ya mabao 6-4 na kupanga kukutana na mabingwa watetezi Paris Saint-Germain katika nusu fainali.
Mchezo ulikuwa sare wakati wa mapumziko katika mechi ya marudiano baada ya kipindi cha kwanza cha kusisimua, huku Real Madrid mabingwa wa Ulaya mara 15 wakiongoza mara tatu katika mchezo huo. Bayern walishinda 2-1 wiki iliyopita Hispania, lakini Arda Guler aliwahi mpira uliopotea kutoka kwa Manuel Neuer na kufunga bao la mapema baada ya sekunde 34 tu katika uwanja wa Allianz Arena. Kisha alifunga tena kwa mpira wa adhabu ndogo baada ya Aleksandar Pavlovic kusawazisha.
Harry Kane aliirejesha Bayern mbele katika jumla ya mabao kabla ya Kylian Mbappe kuisawazishia Real kwa jumla alipofanya iwe 3-2 kabla ya mapumziko.
Eduardo Camavinga alitolewa nje kwa kadi ya pili ya njano zikiwa zimesalia dakika nne, na Bayern wakatumia nafasi hiyo kushambulia, huku Diaz akipiga shuti kali kutoka nje ya boksi lililokwenda wavuni baada ya kugonga mchezaji na kubadilisha mwelekeo.

Real walipokuwa wakisaka bao la kusawazisha, Olise alipiga shuti la kuvutia lililopinda na kuthibitisha ushindi wa Bayern, huku wakidumisha matumaini yao ya kutwaa taji la saba la Ulaya. Watakutana na PSG ya Luis Enrique mwishoni mwa mwezi.
Hasira ziliongezeka baada ya mechi kumalizika, ambapo Guler alipewa kadi nyekundu ya moja kwa moja kwa kumkabili mwamuzi.
“Tulianza vibaya, kisha tukafungwa tena kupitia mpira wa adhabu na shambulizi la kushtukiza. Kipindi cha kwanza kilikuwa na kasi kubwa. Alisema Joshua Kimmich. Kipindi cha pili kilikuwa tulivu zaidi, tulidhibiti mchezo vizuri na hatimaye tukashinda. Haikuwa mechi yetu bora, lakini tunachukua ushindi huo.”
“Timu mbili bora Ulaya zitakutana. Tumekuwa na mechi nyingi kali dhidi ya Paris katika miaka ya hivi karibuni. Natazamia hilo.”
Kipigo hicho kimehitimisha kwa kiasi kikubwa msimu wa Real Madrid, ambao wanaelekea kumaliza bila taji kubwa kwa mwaka wa pili mfululizo. Barcelona wanaongoza La Liga kwa tofauti ya pointi tisa, huku Real pia wakitolewa mapema katika Copa del Rey. Ninawahurumia wachezaji kwa juhudi walizoweka. Inauma,” Alisema kocha Alvaro Arbeloa. “Ninajivunia sana. Tunarudi Madrid baada ya kutoa kila kitu.”

Kwa mara ya kwanza katika historia ya Real Madrid kwenye Ligi ya Mabingwa, kikosi chao cha kwanza hakikuwa na mchezaji hata mmoja Mhispania. Jude Bellingham alikuwa mmoja wa mabadiliko manne yaliyofanywa na Arbeloa.
Neuer, aliyesifiwa kwa kiwango chake katika mechi ya kwanza Madrid, alifanya kosa lililosababisha bao la mapema kwa Real. Golikipa huyo aliupiga vibaya mpira na kumpa Guler, ambaye alifunga kwa shuti la kwanza ndani ya lango tupu.
Bayern walionekana kushangazwa lakini walijibu haraka, Pavlovic akifunga kwa kichwa baada ya Andriy Lunin kushindwa kukadiria mpira vizuri.
Mchezo uliendelea kuwa wa kushambuliana, huku Kane akifunga na Mbappe akijibu. Kane alifunga kwa ustadi dakika ya 38, kabla ya Mbappe kufunga baada ya kupokea pasi kutoka kwa Vinicius Junior na kusawazisha jumla ya mabao kuwa 4-4.


