Hapo jana Sergio Aguero aliweza kupachika magoli mawili ambayo yalikuwa ni ya 200 na 201 kwake ndani ya kikosi cha klabu ya soka ya Manchester City na ikawa ni msaada mkubwa sana wa kuwapatia wao ushindi kwenye gemu ya Ngao ya Jamii wakicheza dhidi ya Chelsea.
City imelamba ushindi wa magoli 2-0 dhidi ya Chelsea ambayo ilishuka dimbani ikiwa chini ya kocha mpya, Maurizio Sarri na ulikuwa ni mchezo ambao ulizikutanisha timu mbili zilizotwaa ubingwa wa Uingereza na ile iliyobeba Kombe la FA msimu wa mwaka jana.
Gemu ilichezwa dimbani Wembley, Uingereza wakati Manchester City wakionekana kutawala sana gemu yote na hiki ni kiashiria kwamba ufunguzi wa Ligi Kuu ya Uingereza unatarajiwa kuanza rasmi mwishoni mwa juma hili.
Hii gemu ya kumkaribisha Sarri imekuwa chungu kwake kabla ya kuanza kwa msimu mpya wakati kiungo mshambuliaji wa City, Bernardo Silva akiwa na siku poa sana kutokana na kuonesha ubora wa hali ya juu na kuwa nguzo kubwa kwenye kumuwezesha Aguero kutupia mabao nyavuni.