Rais wa Marekani Donald Trump ameibua taharuki kubwa kuhusu maandalizi ya Kombe la Dunia la FIFA 2026, akitoa kauli kali kwamba yuko tayari kuhamisha mechi kutoka miji iliyopangwa endapo ataona kuna hatari ya kiusalama. Kauli hiyo imeweka shinikizo kwa Rais wa FIFA Gianni Infantino, ambaye uhusiano wake wa karibu na Trump sasa unazua maswali kuhusu uhuru wa taasisi hiyo ya kimataifa.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Alhamisi, Trump alisema: “Kama nitaona mji si salama, tutahamisha mechi. Bila shaka tutaliamisha Kombe la Dunia. Hatutaruhusu kufanyika katika mji wowote wenye hatari hata kidogo.”
Kauli hiyo imeibua hofu kwamba uingiliaji wa kisiasa unaweza kuvuruga mchakato wa FIFA wa kuchagua miji mwenyeji, mchakato unaojumuisha zabuni, mikataba, ziara za tathmini, na makubaliano ya kimasoko na miundombinu.
Ingawa Chicago haimo kwenye orodha ya miji mwenyeji, Trump alitaja takwimu za uhalifu katika jiji hilo kama mfano wa miji isiyo salama. Hii imefanya wachambuzi waone kuwa miji inayojulikana kama ‘sanctuary cities’ ambapo ushirikiano na maafisa wa uhamiaji wa ICE umepunguzwa inaweza kuwa kwenye hatari ya kuondolewa kwenye ratiba.


