Rais wa Barcelona Joan Laporta amepigwa faini ya Euro 602 kwa kuingia katika chumba cha kubadilishia nguo cha mwamuzi baada ya timu yake kupoteza kwa mbao 3-1 dhidi ya Real Madrid kwenye El Clasico siku ya Jumapili.

Mpaka kumalizika kwa kipindi cha kwanza Barca walikuwa wameshalala kwa mabao 2-0 ambayo yalifungwa na Karim Benzema pamoja na Federico Valverde, na waliporejea kwenye dakika 45 za kumalizia dakika 90 Madrid wailipachika bao la 3 ambalo lilifungwa Rodrygo wakati kwa upande wao Torres ndiye aliwapa bao 1.
Bao la Rodrygo lilifungwa kwa mkwaju wa penati baada ya ukaguzi wa VAR baada ya Eric Garcia kumchezea rafu mchezaji huyo na kufanya Real kuondoka na pointi 3 muhimu zilizopelekea kuongoza ligi.

Matokeo hayo yalizua hisia kali kutoka Rais wa Barcelona Joan Laporta ambaye alishindwa kuvumilia na kwenda kumkabili mwamuzi wa mchezo huo Jose Maria Sanchez Martinez kwenye chumba cha kubadilishia nguo baada ya mechi.
Na baada ya hilo kutokea kamati ya mashindano imemtoza faini Laporta hapo jana huku ikitaja kifungu cha 133 cha kanuni za nidhamu, ambacho kinahusiana na kutofuata maagizo, pamoja na kifungu cha 255, kinachoelekeza wale wanaoingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo wakati hawaruhusiwi kukabiliwa na vikwazo.

Kichapo walichompatia Barca Jumapili kiliwafanya vijana wa Ancellotti kupanda hadi nafasi ya kwanza ya msimamo kwenye Laliga, huku hilo likiwa ni pigo jingine kwa timu ya Laporta baada ya matumaini yao ya Ligi ya Mabingwa kuachwa yakiwa yananing’inia kufuatia sare ya 3-3 nyumbani dhidi ya Inter wiki iliyopita.

