Inaonekana nyota ya mshambuliaji kijana wa Colombia, Jhon Durán, inazidi kufifia kwa kasi, hali inayowaacha mashabiki wa soka wakijiuliza nini kimeenda vibaya kwa kipaji kilichokuwa kikisifiwa sana barani Ulaya.
Takribani miezi 16 iliyopita, Durán alionekana kama mmoja wa washambuliaji vijana wenye mvuto mkubwa zaidi katika Ligi Kuu ya England. Alivutia macho ya wengi baada ya kuibuka na tuzo za Mchezaji Bora wa Mechi katika Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Bayern Munich, kufunga mabao ya kuvutia na kuhusishwa na klabu kubwa kama Chelsea na Arsenal.
Hata hivyo, hali imebadilika kwa kasi isiyotarajiwa. Kwa sasa, Durán anatarajiwa kujiunga na Zenit St Petersburg kwa mkopo, baada ya kupitia mwaka mgumu uliojaa misukosuko na maamuzi yaliyoibua maswali mengi.
Baada ya kuhamia Saudi Arabia, mshambuliaji huyo alidumu kwa miezi sita pekee kabla ya kuondoka Al-Nassr, kufuatia kutofautiana kimtazamo na nyota mkubwa Cristiano Ronaldo pamoja na uongozi wa klabu. Hatua hiyo ilichukuliwa kama pigo kubwa kwa maendeleo yake.




