YANGA tayari imefanikiwa kumtangaza winga machachari Bernard Morrison kuwa ni mchezaji wao mpya ndani ya timu hiyo jambo ambalo limeibua shangwe jingi kwa mashabiki wa Yanga ambao wameanza kutamba kuwa kwa usajili huo utawafanya watambe msimu ujao katika michuano ya kimataifa.
Yanga ukiachana na Morrison tayari imeshamtambulisha mshambuliaji mwingine wa pembeni Lazarous Kambole ambaye alikuwa akikipiga katika klabu ya Kaizer Chiefs ya nchini Afrika Kusini.
Ukiachana na wachezaji hao pia Yanga ni wazi tayari wamekamilisha usajili wa kiungo mshambuliaji wa timu ya taifa ya Burkinafaso Aziz Ki ambaye wanayanga wanaamini mchezaji huyo atatambulishwa hivi karibuni.
Kama ambavyo kocha Nasreddine Nabi ambaye amekuwa ni muumini wa mfumo wa 4-2-3-1 au 3-5-2 ni wazi kuwa usajili wa wachezaji hao wawili yaani Morrison na Azizi ki watakwenda kusuka utatu mtakatifu katika kikosi kipyacha Yanga kwa msimu ujao wakishirikiana na mshambuliaji wa kati Fiston Mayele ambaye tayari ameuteka ufalme ndni ya Yanga.
Hivyo katika mfumo wa 4-2-3-1 Morrison anategemewa kutokea katika upande wa kushoto yaani winga namba 11 huku Aziz Ki akitegemewa kutokea katika upande wa kulia yaani namba saba huku Fiston Mayele akicheza kama namba 9 akicheza kati na Feisal Salum akicheza namba 10.
Hata hivyo Yanga pia itakuwa na machaguo mengi katika kikosi chao msimu ujao kwani ni kulingana na kuwa na wachezaji wengi wenye uwezo mkubwa wa kucheza katika nafasi nyingi ofauti tofauti.
Miongoni mwa wachezaji hao ni pamoja na Aziz Ki ambaye anaweza kucheza nafasi zote za kiungo mshambuliaji kama winga wa kulia,winga wa kushoto na kiungo mshambuluiaji yaani namba 10 huku pia Bernard Morrison akiwa na uwezo wa kucheza wing azote za kulia na kushoto na pia kama namba 10.
Kwa upande wa Feisal Salum pia anauwezo wa kucheza kama namba 10 na namba 8 jambo ambalo ni wazi ni faida kubwa kwa Yanga kuelekea katika michuano ya kimataifa ambayo msimu uliopita hawakufanya vizuri.
Makamu mwenyekiti wa kamati ya Mashindano Yanga Injinia Hersi Said alisema kuwa “Kuelekea katika msimu ujao wa kimataifa Yanga tunamalengo makubwa ya kufanya vizuri tofauti na msimu uliopita ambapo tulifanya vibaya.
“Yanga kwa usajili ambao tutaufanya msimu huu utatusaidia kwa kiasi kikubwa kwakuwa tunaamini wachezaji hao wengi wanauwezo mkubwa na wanauzoefu katika michuano hiyo lakini pia kutakuwa na maelewano mazuri tofauti na msimu uliopita ambapo wachezaji wengi walikuwa ni maingizo mapya katika kikosi chetu,”alisema kiongozi huyo.