BAADA ya kuteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Yanga (CEO), Andrew Mtine amefunguka kuwa amechagua kufanya kazi ndani ya klabu hiyo kutokana na historia kubwa ya klabu hiyo.
Mtine ametambulishwa na Uongozi wa Yanga kupitia kwa Rais wa Yanga, Eng. Hersi Said leo akichukua nafasi ya Senzo Mazingisa ambaye aliomba kuondoka ndani ya klabu hiyo.
Miongoni mwa nafasi ambazo amewahi kuzitumikia ni pamoja na klabu ya TP Mazembe kwa miaka 12, pia alifanya kazi akiwa Mjumbe wa kamati ya fedha ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Mtine ambaye ni raia wa Zambia amesaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia klabu ya Yanga katika nafasi hiyo.
Akizungumza baada ya kutambulishwa, Mtine amesema kuwa “Ni heshima kubwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Yanga, najua Yanga ina historia kubwa ndio maana nimechagua kufanya kazi hapa, natambua nafasi kubwa ya wale wote ambao wamefanya kazi kubwa ya kuifikisha Yanga hapa ilipo.”