Ligi Kuu ya NBC kuendelea hii leo kwa michezo miwili ambapo mchezo wa mapema kabisa ni ule unaowakutanisha Tanzania Prisons dhidi ya Namungo kutoka mkoani Lindi na baadae kufuatiwa na mchezo wa Geita Gold dhidi ya Yanga.

Mchezo huo unatarajiwa kupigwa mapema kwenye majira ya saa 8:00 mchana katika uwanja wa Sokoine jijini Mbeya ambapo mwenyeji wa mchezo huo atakuwa ni Tanzania Prisons (Wajelajela).
Prisons wamecheza michezo 8 mpaka sasa, huku wakiwa wameshinda michezo mitatu, wametoa sare tatu na pia wamepoteza michezo miwili kwenye Ligi mpaka sasa. Wakati kwa upande wa Namungo wao wamecheza michezo 8 pia, ushindi mara nne, sare mbili na kupoteza michezo miwili.

Timu zote zinakutana hii leo baada ya kushinda mechi zao za mwisho wakati Tanzania Prisons yupo nafasi ya 9 akiwa na pointi 12, Na Namungo akiwa nafasi ya 5 na kujikusanyia pointi 14 mpaka sasa.
Mechi 5 za mwisho kukutana hizi timu mbili Prisons ameshinda mara 2 na wametoa sare 3 wakati Namungo hajapata matokeo ya ushindi hata mechi moja. Na kila mmoja leo anahitaji matokeo ya alama tatu.


